Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, amesema kuwa chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Serikali imeimarisha mazingira ya walimu kwa kujenga na kuboresha miundombinu ya shule hali iliyoongeza ufanisi wa ufundishaji na ujifunzaji.



Prof. Nombo ameeleza kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia inasimamia utekelezaji wa sera ya elimu, elimu msingi, mafunzo ya ualimu tarajali na mafunzo endelevu kwa walimu kazini, jambo linaloonesha uzito wa nafasi ya walimu katika sekta ya elimu.



Aidha, kupitia mpango wa mafunzo endelevu kwa walimu kazini (MEWAKA), walimu wamepata mafunzo ya kitaaluma katika maeneo ya utekelezaji wa mitaala, ufundishaji wa masomo ya sayansi, hisabati, TEHAMA, tathmini, usawa wa kijinsia na ujumuishi, hatua iliyoimarisha umahiri wao.



Prof. Nombo amesema kuwa Serikali kupitia Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014/2023, imeandaa mkakati wa kuboresha mazingira ya kazi na maslahi ya walimu ngazi zote za elimu na inaendelea kusimamia utekelezaji kwa kushirikiana na wadau wakiwemo Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET).



Pia Wizara imeanzisha programu ya Leaders in Teaching inayolenga kuimarisha mbinu za ufundishaji, kutoa mafunzo ya ujasiriamali kwa walimu na kuongeza motisha ili kuboresha elimu nchini.