Serikali imesema imefanikiwa kuondoa changamoto ya wizi wa mitihani iliyokuwa inaanzia ndani ya Baraza la Mitihani la Tanzania.



Hayo yamesemwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda Machi 15, 2024 Jijini Dar es Salaam wakati Kamati ya Kudumu ya Elimu, Utamaduni na Michezo ilipotembelea Baraza hilo ambapo amesema kwa sasa serikali inaendelea kupambana na wizi wa mitihani wa kitaasisi kwa kushirikiana na watumishi wa serikali wasiokuwa waaminifu.



Aidha, Waziri huyo ameongeza kuwa changamoto kubwa kwa sasa ni kuchelewa kwa kesi kwani zinakaa muda mrefu, lakini bado serikali inaendelea kupambana na wizi wa mitihani.



Akizungumzia kuhusu suala la mdondoko wa wanafunzi, waziri huyo amesema serikali imeunda kamati mbili ambazo moja inajukumu la kufuatilia mabinti waliopata ujauzito na kurudi shuleni kufahamu changamoto wanazokutana nazo na masuala mengine kuhusu maendeleo yao kielimu na kamati ya pili inaangalia mfumo mzima wa takwimu za elimu nchini ili kuwa na takwimu sahihi katika mfumo mzima wa elimu.