Serikali ya Tanzania inatekeleza kwa vitendo mikataba mbalimbali ya Kimataifa na Kikanda inayohusu Elimu Jumuishi na lengo Namba 4 la Malengo Endelevu ya Milenia ya Mwaka 2030 linalosisitiza utoaji wa elimu kwa usawa.

Kauli hiyo imetolewa Septemba 17, 2024 jijini Arusha na Waziri wa Nchi, ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Mohamed Mchengerwa wakati akifungua Maadhimisho ya Miaka 30 ya Elimu Jumuishi.

"Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekua ikiandaa Sera, miongozo na mikakati mbalimbali ukiwemo Mkakati wa Kitaifa wa Elimu Jumuishi wa mwaka 2022-2026 unaolenga kufanikisha utoaji wa Elimu na ujenzi wa utamaduni jumuishi ndani na nje ya shule" Alisema Mchengerwa.

Mhe. Mchengerwa amesema katika kipindi cha mwaka 2022/23 na 2023/24, Serikali imetoa zaidi ya Shilingi bilioni 8.3 kwa ajili ya kununua na kusambaza vifaa maalumu na vifaa saidizi kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalumu katika Taasisi za elimu.

Amewataka Viongozi wote wa Mikoa na Halmashauri Nchini kusimamia kwa dhati na kwa wakati zoezi la ubainishaji na utambuzi wa awali wa watoto ili kubaini wenye mahitaji maalum.

#UzinduziMaadhimishoMiaka30ElimuJumuishi
#ElimuUjuziMpangoMzima
#TunaboreshaElimuYetu
#Kaziiendelee