Njombe yajivunia kupata Kampasi ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kinachojengwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) ambayo itakuwa Taasisi ya Kwanza ya Elimu ya Juu katika mkoa huo.

Akizungumza Septemba 20, 2024 mkoani Njombe wakati wa kuanza kwa ziara ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita, Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Deo Mwanyika amesema kuwa uamuzi wa ujenzi wa kampasi hiyo utakuwa mkombozi kwa wananjombe  kupata elimu ya Juu.

Kwa Upande wake Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma Taaluma Prof.  Razack Lokina amesema ujenzi wa Kampasi hiyo utaanza Disemba 2024, utagharimu shilingi bilioni 20 na ujenzi ukikamilika chuo kinatarajiwa kuchukua wanafunzi 1000 na kitaanza kwa kutoa kozi za stashahada na shahada za ujuzi katika fani za kilimo, TEHAMA, Misitu pamoja na mazao yake na zingine zinazoendana na shughuli za kiuchumi za Mkoa wa Njombe .

#SamianaMaendeleo